Idara ya Ardhi Mkoa wa Ruvuma imepokea vifaa mbalimbali vya TEHAMA ikiwemo kompyuta 24, UPS 24, printer kubwa 8, skana kubwa 3 na simu za IP 6 ikiwa ni sehemu ya jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita katika kuboresha utoaji wa huduma, kuongeza uwazi, ufanisi na kasi ya kuhudumia wananchi kupitia mifumo ya kidijitali.
Akikabidhi vifaa hivyo kwa Maafisa Ardhi wa Mkoa wa Ruvuma, Kamishna wa Ardhi Msaidizi Mkoa wa Ruvuma, Bw. Saidi Juma Kijiji, amewataka maafisa hao kuhakikisha wanavitumia kwa manufaa ya wananchi. Akisisitiza kuwa dhamira ya serikali ni kurahisisha kazi na kuongeza ufanisi katika sekta ya ardhi, hivyo jukumu la kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora linabaki kwa maafisa husika.
Bw. Kijiji amewahimiza maafisa hao kufanya kazi kwa bidii hususan katika utoaji wa hati miliki, ukadiriaji wa kodi na kupima viwanja kwa urahisi na kwa muda mfupi.
Kwa upande wake, Afisa Ardhi Mteule kutoka Ofisi ya Kamishna wa Ardhi Msaidizi Mkoa wa Ruvuma ameishukuru serikali kupitia Wizara ya Ardhi kwa kuwapa vitendea kazi. Amesema kuwa vifaa hivyo vitakuwa chachu ya utekelezaji wa majukumu ya kila siku na vitawawezesha kutoa huduma kwa ufanisi zaidi.
Naye Msimamizi wa Sekta ya Ardhi Wilaya ya Nyasa, Bw. Phileteus Komba, amebainisha kuwa changamoto kubwa iliyokuwa ikiwakabili ni upungufu wa vitendea kazi. Hivyo vifaa walivyokabidhiwa vitawawezesha kufanya kazi kwa wakati na kwa ufanisi, na kuboresha huduma kwa wananchi wa wilaya hiyo.
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.