Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini ambayo hufanyika Februari 2 kila mwaka, katika mkoa wa Ruvuma yamefanyika katika viwanja vya Mahakama Kuu Kanda ya Songea, yakiongozwa na kaulimbiu isemayo “Mchango wa Mahakama katika Ustawi wa Maendeleo ya Taifa.”
Akizungumza katika maadhimisho hayo, Jaji Mfawidhi wa Kanda ya Songea, Mhe. James Karayemaha, amesema Mahakama ya Tanzania ni chombo pekee chenye mamlaka ya mwisho ya kutoa haki hivyo ina wajibu mkubwa wa kusimamia haki.
Amesema mahamaka inaendelea kutoa elimu kwa jamii kuhusu sheria na haki za wananchi kupitia mitandao ya kijamii na vyombo vya habari. Akibainisha kuwa hatua hiyo imeongeza uelewa wa wananchi juu ya taratibu za kisheria na haki zao.
Ameeleza kuwa mwaka 2025 Mahakama iliweka mkakati maalum wa kusikiliza mashauri 2,128 ya kimkakati yanayohusu biashara, kodi, benki, ardhi na uwekezaji, yaliyokuwa yameshikilia zaidi ya shilingi trilioni 9 na bilioni 400 ambapo mkakati huo ulitekelezwa kuanzia Novemba 10 hadi Desemba 4, 2025, na kufanikisha kumaliza mashauri 1,527 sawa na asilimia 72.
Mhe. Karayemaha amebanisha kuwa Katika Kanda ya Ruvuma pekee, mashauri 22 yaliingizwa kwenye mpango huo na 19 kati yake yakamalizika, sawa na asilimia 86, hatua iliyosaidia kufungua shughuli za kiuchumi zilizokuwa zimesimama.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama cha Mawakili wa Kujitegemea Mkoa wa Ruvuma, Elseusi Ndunguru, amesema kaulimbiu ya mwaka huu inaonyesha kuwa hakuna maendeleo ya kweli bila ulinzi wa haki, utawala wa sheria na misingi ya utawala bora. Akisisitiza kuwa Mahakama ni nguzo muhimu katika kuhakikisha ustawi wa taifa na maendeleo endelevu.
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.