Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Brigedia Jenerali Ahmed Abbas Ahmed, ameipongeza Shule ya Sekondari ya Wavulana Kigonsera kwa utekelezaji wa elimu ya kujitegemea pamoja na miradi ya maendeleo inayotekelezwa kupitia mapato yanayotokana na programu hiyo.
Akizungumza wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua miradi ya shule hiyo wilayani Mbinga, Brigedia Jenerali Ahmed amesema shughuli zinazotekelezwa zina manufaa makubwa kwa shule, wanafunzi na wazazi ambao wamekuwa wakijitolea kuchangia fedha ili kuendeleza miradi hiyo.
Pamoja na mambo mengine amemuagiza Mkuu wa Wilaya ya Mbinga na Mkurugenzi wa Halmashauri kuhakikisha wanajenga barabara ya lami inayoingia shuleni hapo, akisistiza kuwa hatua hiyo itaheshimu historia kubwa ya shule hiyo ambayo imezalisha viongozi wakuu wa taifa.
Naye Katibu Tawala wa Mkoa wa Ruvuma, Bi Mary Gasper Makondo, amesema shule hiyo imekuwa shamba darasa kwa shule nyingine ambazo hujifunza kupitia miradi yake. Amesisitiza umuhimu wa kuendeleza ubunifu na kuboresha miradi ili matokeo yawe makubwa zaidi.
Kwa upande wake, Mwalimu Mkuu wa shule hiyo, Ponsiano Ngungulu, amesema mpango wa elimu ya kujitegemea ulianza mwaka 2012 kwa miradi mitatu pekee, lakini kufikia Januari 2026 shule hiyo inatekeleza jumla ya miradi 11.
Miradi hiyo ni pamoja na kilimo cha mahindi, bustani ya mboga na migomba, ufugaji wa ng’ombe, samaki, kuku wa nyama, nyuki, pamoja na mashine ya kusaga nafaka na kuongeza virutubisho pamoja na kujenga nyumba za watumishi.
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.