Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Brigedia Jenerali Ahmed Abbas Ahmed, amefanya ziara ya kukagua ujenzi wa masoko ya Manzese A na B pamoja na Soko la Bombambili, manispaa ya Songea. Katika ziara hiyo, ameonyesha kutoridhishwa na kasi ya utekelezaji wa ujenzi wa masoko hayo pamoja na mazingira ya Soko la Bombambili.
RC Ahmed amesema kuwa hadi sasa ujenzi wa masoko ya Manzese A na B haujaanza licha ya mkandarasi kulipwa shilingi bilioni 3 kama malipo ya awali. Mradi huo ulipangwa kuanza Julai 15, 2025 na kukamilika Julai 12, 2026, lakini eneo husika limewekewa uzio pekee bila hatua za ujenzi kuanza.
Ameagiza mkandarasi kuwasilisha barua rasmi ofisini kwake, ikionyesha namna atakavyoharakisha utekelezaji wa mradi huo ili kuhakikisha unakamilika kwa wakati na kuondoa changamoto zinazoweza kuathiri mpango wa Manispaa ya Songea wa kukusanya ushuru.
Kwa upande wa Soko la Bombambili, ambalo linaendelea kutoa huduma, RC Ahmed amesema mazingira yake ni mabovu na hayaridhishi. Ameelekeza barabara zote zinazoingia sokoni zirekebishwe bila gharama, taka ziondolewe mara moja, na kuwepo usimamizi mzuri wa malori ili kuepusha uharibifu wa barabara baada ya matengenezo.
Amesisitiza kuwa maelekezo hayo yatekelezwe ndani ya wiki moja, akionya kuwa kipindi cha mvua kinaweza kusababisha magonjwa ya mlipuko kama kipindupindu endapo mazingira hayatadhibitiwa.
RC Ahmed ameongeza kuwa masoko yaliyopo sasa hayana mazingira mazuri, hivyo wananchi na wafanyabiashara wanakabiliwa na changamoto kubwa ya kufanya shughuli zao katika hali isiyo rafiki.
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.