Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Brigedia Jenerali Ahmed Abbas Ahmed, amesema katika kukabiliana na hali ya lishe duni Mkoa wa Ruvuma utaanza kutekeleza mpango harakishi, shirikishi na jumuishi wa kupunguza udumavu katika maeneo yote ya Mkoa.
Akifungua kikao cha tathimini ya mkataba wa lishe kwa mwaka wa fedha 2024/2025 kwa Mkoa wa Ruvuma, kilichofanyika katika ukumbi wa Songea Club mjini Songea, Brig. Jen. Ahmed amesema mpango huo utatekekezwa kwa miaka mitano kuanzia mwaka huu wa fedha wa 2025/26.
"Mkoa utaanza kutekeleza mpango harakishi, shirikishi na jumuishi wa kupunguza udumavu katika maeneo yetu kwa miaka mitano kuanzia mwaka huu wa fedha 2025/26 katika halmashauri zetu zote kwa kutumia rasilimali tulizonazo ili kubaini visababishi vinavyofanya uwepo wa hali duni ya lishe," alisema Brig. Jen. Ahmed.
Hata hivyo amesema kwa kuwa visababishi vya lishe duni ndani ya mkoa vinajulikana ametoa ushauri kwa wataalam kuchukua hatua za utekelezaji wa utatuzi wa tatizo hilo huku wakiendelea na tafiti kwa hatua zaidi na matokeo chanya.
Katika hatua nyingine amesisitiza kuimarisha huduma ya upatikanaji wa chakula mashuleni kwani huduma hiyo bado haitolewi kikamilifu na shule zingine zinatoka chakula lakini idadi ya wanafumzi wanaopata chakula ni idadi ndogo.
Naye Katibu Tawala wa Mkoa wa Ruvuma, Bi Mary Makondo, amesema Ruvuma ni kati ya mikoa inayokabiliwa na changamoto ya lishe licha ya kuzalisha vyakula vya makundi mbalimbali, hivyo kwa mkakati ulioandaliwa ambao utatekelezwa kwa miaka mitano utasaidia kuondoa changamoto ya udumavu katika mkoa.
Kwa upande wake Afisa Lishe Mkoa wa Ruvuma, Joyce Kamanga, amebainisha mikakati ya kupambana na changamoto ya lishe ambayo ni halmashauri kuhakikisha zinatoa fedha za lishe kila robo mwaka, halmashauri kupitia wahudumu wa afya na maafisa lishe kuendelea kutoa Elimu ya lishe kuhusu siku 1,000 ili kupunguza tatizo la watoto wanaozaliwa na uzito pungufu au lishe duni.
Mikakati mingine ni kuhakikisha halmashauri zinatenga fedha kwa ajili ya kununua virutubishi vya kuongeza kwenye unga wa mahindi pamoja na kuwahamasisha wazazi kuchangia chakula mashuleni.
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.