Mkoa wa Ruvuma umeanza hatua za dharura kukabili hali duni ya lishe, baada ya takwimu za 2022 kuonesha udumavu wa watoto chini ya miaka mitano kufikia asilimia 35.6 kiwango kilicho juu ya wastani wa kitaifa.
Mkuu wa Mkoa Brig. Jen. Ahmed Abbas Ahmed amesema juhudi za kisera, kijamii na kiafya zinaimarishwa ili kulinda afya ya mama na mtoto.
Kwa sasa, mkoa unatekeleza mkakati kabambe wa lishe 2025/26, ukijumuisha mashine 69 za kurutubisha unga wa mahindi, elimu ya lishe kwa zaidi ya wazazi/waangalizi 99,771, utoaji wa vidonge vya kuongeza damu kwa asilimia 90 ya wajawazito, pamoja na matibabu jumuishi ya utapiamlo mkali. Zaidi ya 3,142 kati ya 3,268 shule zina klabu za lishe zinazowahimiza watoto kula chakula cha mchana na kuanzisha bustani za mboga na matunda.
Aidha, watoto 121 waliogunduliwa na utapiamlo mkali wamehudumiwa, ambapo 109 walipona. Serikali ya mkoa imetumia Sh bilioni 0.534—sawa na asilimia 92 ya bajeti—kutekeleza afua za lishe katika kipindi cha 2024/25.
Mkoa unaamini hatua hizi zitaipandisha Ruvuma kutoka kwenye ramani ya udumavu kwenda kwenye kizazi chenye afya na uwezo wa kujifunza.
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.