Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Brigedia Jenerali Ahmed Abbas Ahmed, amesema walimu ni nguzo ya mabadiliko ya kijamii, kiuchumi na kiutamaduni katika taifa akisisitiza kuwa taifa linalotaka kupiga hatua lazima liwekeze kwa dhati katika walimu wake.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mkutano wa walimu wa kanda ya kusini na mashariki (SETCO) uliofanyika mjini Songea katika ukumbi wa Chandamali, Brig. Jen. Ahmed amesema walimu ndio wapandaji wa mbegu ya elimu akifafanua kuwa mbegu hiyo ikiachwa bila ufuatiliaji inaweza kudhoofika, hivyo ni muhimu kufuatilia changamoto mapema na kuchukua hatua za haraka.
Amesema serikali imefanya kazi kubwa kuboresha mazingira na miundombinu ya kufundishia na kujifunzia, kwa kutambua kuwa walimu bora wanahitaji mazingira bora ili kutoa matokeo bora. Hivyo ni lazima uwekezaji huo uonekane kwa matokeo halisi ya ufaulu wa wanafunzi.
Brigedia Jenerali Ahmed Abbas amewataka walimu wote kuweka mpango wa kuinua matokeo ya somo analofundisha, huku wakifanya ufuatiliaji na tathmini ya mara kwa mara. Akiwaagiza viongozi wa shule kuhakikisha kunakuwa na ufuatiliaji endelevu wa ufundishaji, mahudhurio ya wanafunzi na matumizi ya vifaa vya kujifunzia.
Kwa upande wake, Rais wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT), Dkt. Sulemani Ikomba, amesema kumekuwa na changamoto kadhaa katika halmashauri ambazo madiwani wa kila kata wanapaswa kuzitatua.
Ameeleza kuwa bajeti zimetengewa kwa ajili ya kushughulikia changamoto za walimu ikiwemo matibabu, hivyo madiwani wanapaswa kuhakikisha walimu wanapata msaada wanapokumbwa na matatizo ya kiafya ili waweze kurejea kazini kwa haraka.
Akisoma risala kwa mgeni rasmi, Katibu wa CWT Wilaya ya Mbinga, Mwalimu Chacha Maro, ametaja miongoni mwa changamoto wanazozipata walimu ni sheria ya kikokotoo ambayo imekuwa ikiwakwamisha walimu kupata maslahi bora.
Amebainisha kuwa walimu wamekuwa wakicheleweshewa kulipwa madeni yao na pia kuna upungufu mkubwa wa walimu. Ameiomba serikali kuajiri walimu kwa kasi ili kupunguza changamoto hiyo.
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.