Serikali ya awamu ya sita imewezesha mradi wa upatikanaji wa matrekta matano (5) kwa ajili ya kuimarisha sekta ya kilimo katika halmashauri ya Wilaya ya Songea, ikiwa ni mkakati kutoka Serikali kuu kupitia Wizara ya Kilimo, kwa lengo la kuongeza uzalishaji wa mazao, kupunguza gharama za uzalishaji na kuboresha maisha ya wakulima wadogo.
Akizungumza mara baada ya kupokea matrekta hayo, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Songea, Bi. Elizabeth Gumbo, alisema kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Songea ni miongoni mwa Halmashauri zinazotegemea kwa kiasi kikubwa kilimo kama mhimili wa uchumi wa wananchi wake, hivyo ujio wa zana hizo za kisasa za kilimo ni chachu muhimu ya maendeleo kwa wakulima.
Bi. Gumbo alieleza kuwa uwepo wa matrekta hayo utawezesha wakulima kulima kwa wakati, kuongeza ukubwa wa mashamba, kuinua uzalishaji na hatimaye kuongeza kipato cha kaya nyingi za wakulima.
Aidha, alimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluh Hassan, lakin pia Waziri wa Kilimo na Wizara ya Kilimo kwa kuendelea kuiwezesha Halmashauri hiyo kwa zana za kisasa za kilimo, ikiwa ni sehen ya kumuinua mkulima mdogo na kuendeleza sekta ya kilimo nchini.
“Matrekta haya yatakwenda kubadili kabisa taswira ya kilimo katika Wilaya yetu, Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuona umuhimu wa kuwekeza kwenye kilimo na kumfikia moja kwa moja mkulima wa kawaida,” alisema Bi. Gumbo.
Matrekta hayo yamegawanywa katika kata mbalimbali ndani ya Halmashauri ya Wilaya ya Songea ili kuhakikisha wakulima wengi zaidi wananufaika kulingana na mahitaji ya maeneo yao.
Katika juhudi za kushuhudia utekelezaji wa mradi huo kwa vitendo, Kitengo cha Mawasiliano Serikalini kilitembelea Kata ya Mpitimbi, ambayo ni miongoni mwa kata zilizonufaika na mradi huo.
Wakulima wadogo wadogo kutoka kata hiyo walieleza kufurahishwa kwao na hatua ya Serikali ya Awamu ya Sita kuwekeza katika zana za kisasa za kilimo, wakisema kuwa matumizi ya matrekta yameleta mapinduzi makubwa katika shughuli zao za kilimo ikilinganishwa na kilimo cha jembe la mkono.
Miongoni mwa wanufaika wa mradi huo ni Bi. Celina Ngonyani na Bi. Prisca Komba, wakulima kutoka Kata ya Mpitimbi, ambao walilimiwa mashamba yao kwa kutumia matrekta hayo. Wamesema kuwa gharama za kulima kwa trekta ni nafuu zaidi, huku wakiweza kulima maeneo makubwa kwa muda mfupi, jambo linaloongeza uzalishaji na kipato chao.
“Mradi huu umetusaidia sana sisi wakulima wadogo zamani tulitumia muda mwingi na nguvu nyingi kulima kwa jembe la mkono, lakini sasa trekta linatulimia haraka na kwa gharama nafuu,” alisema Bi. Celina kwa furaha.
Kwa upande wake, Bi. Prisca alimshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kumuona na kumthamini mkulima mdogo, akisema kuwa mradi huo umeongeza ari ya kufanya kilimo cha kibiashara badala ya kilimo cha kujikimu pekee.
Akizungumza kuhusu utaratibu wa upatikanaji wa zana hizo za kilimo, Mratibu wa zana za kilimo katika Halmashauri ya Wilaya ya Songea, Bw. Mathias Ambros, alisema kuwa mkulima yeyote anayehitaji kulimiwa shamba lake anatakiwa kumuona Afisa Kilimo wa Kata husika na kuwasilisha maombi rasmi, au kuwasiliana moja kwa moja na mratibu wa zana hizo kupitia namba ya simu 0688 273 176 ili kuratibiwa huduma hiyo.
Mradi wa matrekta ni miongoni mwa vielelezo vya dhamira ya dhati ya Serikali ya Awamu ya Sita katika kuboresha sekta ya kilimo kama mhimili wa uchumi wa Taifa, sambamba na azma ya Rais Samia ya kuhakikisha wananchi, hususan wa vijijini, wananufaika moja kwa moja na miradi ya Serikali.
Wananchi wa Halmashauri ya Wilaya ya Songea wameendelea kupongeza uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa maamuzi yake ya kuwekeza katika kilimo, wakisema kuwa mradi wa matrekta ni ushahidi wa falsafa ya “Kazi na Utu, Tunasonga Mbele” na dhamira ya kujenga uchumi imara unaomuinua mkulima
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.