Katika hekaheka za kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwaka huu, ujumbe mmoja umesimama imara kama mnara wa taa katika giza nene ni ule alioutoa Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Stephen Wasira, akiwa katika wilaya ya Tunduru, Mkoa wa Ruvuma.
Katika kikao cha ndani kilichowakutanisha wanachama wa CCM, viongozi wa dini, na makundi mbalimbali ya kijamii, Wasira hakuacha shaka: “Watanzania, jiandaeni kutiki. Tiki kubwa kabisa kwa Rais Samia Suluhu Hassan na mgombea mwenza wake, Dk. Emmanuel Nchimbi.”
Katika ulimwengu wa siasa unaotikiswa na kauli tata kama "No Reform No Election", Wasira ameweka wazi kuwa hakuna kikundi, mtu, wala kaulimbiu inayoweza kuzuia uchaguzi wa kidemokrasia nchini Tanzania.
Samia: Kiongozi wa Maridhiano
Wasira hakusita kumwelezea Rais Samia kama chombo cha maridhiano kilichosafisha njia ya maelewano miongoni mwa vyama vya siasa nchini.
Amesema Katika kipindi cha miaka minne ya uongozi wake,Rais Samia amejitahidi kusikiliza kila upande hata wale waliotaka kusikika wao tu.
“Hata CHADEMA waliposita, Rais Samia aliwasikiliza. Haya si maneno, ni historia ya kweli,” alisema Wasira kwa msisitizo.
Kauli hiyo iliambatana na mfano halisi wa matukio: “Juzi tu Mnyika alienda Kondoa kuhubiri ‘No Reform No Election’. Lakini wananchi wakamwambia macho macho tunaenda kutiki Oktoba.” Kwa maneno hayo, Wasira aligeuza sintofahamu kuwa uamuzi thabiti wa wananchi kuitikia wito wa uchaguzi kwa ari.
Uongo ni Giza, Ukweli ni Umeme
Wasira, mwanasiasa mwenye uzoefu wa miongo kadhaa, alitumia taswira nzito kuelezea mapambano kati ya propaganda na ukweli: “Uongo unafanana na giza, na ukweli unaogopwa na uongo kama vile giza linavyoogopa umeme.
Aliongeza kuwa kazi ya viongozi ni kuwasha umeme huo kwa wananchi kwa kuwapa elimu, uelewa na hamasa ya kushiriki uchaguzi.
Tanzania: Nchi ya Amani na Umoja wa Kweli
Katika kipengele kilichogusa mioyo ya wengi, Wasira alisisitiza kuwa Tanzania ni nchi ya nadra barani Afrika nchi inayosimama kwa amani, umoja na mshikamano. Alisema, “Afrika ina matatizo mengi, lakini Tanzania haijawahi kushuhudia mapinduzi ya kijeshi, vita vya wenyewe kwa wenyewe, wala machafuko ya kisiasa. Huu ni ushahidi wa kazi nzuri iliyofanywa na chama chetu na viongozi wake.”
Aliendelea kueleza kuwa dini si chanzo cha migogoro nchini. Kwa kutumia mfano wa Ibrahimu, chimbuko la dini zote kuu, alisema, “Ibrahim kasema tugombane? Hapana. Mungu mmoja ametuita tumwabudu, si tugombane.”
CCM: Chama Kilichojenga Msingi Imara
Kwa mujibu wa Wasira, tofauti ya CCM na vyama vingine iko wazi: ni chama kilichojenga msingi wa amani na maendeleo kwa miaka zaidi ya 60. “Hatutaki ugali wa jana kama kiporo, tunataka ugali wa moto unaotoa moshi maendeleo yanayoonekana, yanayogusa maisha ya watu.”
Alimnukuu Rais Mstaafu Dk. Jakaya Kikwete aliyewahi kusema, “Nchi haiwezi kupoa kama ugali wa jana,” akimaanisha kuwa maendeleo lazima yawe endelevu na yenye msukumo wa sasa.
Tiki Siyo Tena Alama—Ni Dhamira ya Taifa
Hotuba ya Wasira ni mwaliko wa kuchagua si tu wagombea, bali mustakabali wa taifa.Na kama alivyoeleza kwa sauti ya mwisho:“Msibabaishwe nenda mkapige kura.
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.