Maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika kimkoa yaliyofanyika Juni 16, 2025, katika Halmashauri ya Madaba, wilayani Songea, yamesisitiza umuhimu wa jamii, Serikali, wazazi na wadau wote kuungana kuwalinda, kuwatunza na kuwaendeleza watoto, kama hazina ya taifa la kesho.
Hafla hiyo, iliyohudhuriwa na mamia ya wananchi, iliongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Namtumbo, Mheshimiwa Ngollo Malenya, aliyemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Kanali Ahmed Abbas Ahmed.
Katika hotuba yake, Malenya aliwakumbusha Watanzania historia ya Siku ya Mtoto wa Afrika, inayotokana na maandamano ya watoto wa Soweto, Afrika Kusini, Juni 16, 1976, maandamano yaliyokuwa yakipinga mfumo wa elimu wa kibaguzi na hatimaye kusababisha vifo, kujeruhiwa, na mateso ya mamia ya watoto.
“Siku ya Mtoto wa Afrika ni fursa ya pekee ya kutafakari; tulipotoka, tulipo, na tunapoelekea. Kauli mbiu ya mwaka 2025,Haki za Mtoto: Tulipotoka, Tulipo na Tuendako inatukumbusha sote kuwa mustakabali wa watoto upo mikononi mwetu. Tukiwekeza kwa watoto, tunawekeza kwa taifa zima.” Alisisitiza Malenya.
Takwimu za Sensa ya Watu na Makazi ya 2022 zinaonesha mkoa wa Ruvuma una watoto 855,106, wakiwakilisha asilimia 46.3 ya idadi ya watu 1,848,794. Kati ya watoto hao, wavulana ni 428,058 na wasichana 427,048.
Takwimu hizo zinabainisha dhahiri wajibu wa jamii na Serikali kutoa kipaumbele kwa malezi, ulinzi, elimu, na afya ya watoto.
Serikali, kupitia Sera ya Maendeleo ya Mtoto ya 2008, Sheria ya Mtoto Na. 21 ya 2009 (pamoja na marejeo ya 2019), madawati ya ulinzi wa watoto, na Programu ya Shule Salama, imetenga rasilimali na mifumo ya kisheria inayolenga kuhakikisha watoto wanapata haki ya kuishi, kupendwa, kulindwa, kutobaguliwa, kuendelezwa, na kushirikishwa.
Akihutubia umati wa wananchi, Malenya alisisitiza: “Serikali ya Tanzania inatekeleza sera hizi kwa vitendo. Majengo ya madarasa, madawati ya ulinzi, dawati la jinsia na watoto, huduma za afya, na ruzuku ya elimu ni mifano hai ya jinsi Serikali inavyothamini maisha ya watoto.”
Hata hivyo, Malenya alibainisha changamoto zinazoukabili mkoa, kama vile baadhi ya wazazi kutowajibika, watoto kuishi mitaani, na kuongezeka kwa visa vya ukatili.
Alitolea mfano wa takwimu za Polisi mkoani Ruvuma, zinazonesha kwamba takriban visa 30 hadi 40 vya ukatili wa kingono huripotiwa kila mwaka, lakini vingi havifikishwi mahakamani kutokana na ushirikiano mdogo wa familia.
“Tunawasihi wazazi, walezi na jamii nzima, tusifumbie macho vitendo vyovyote dhidi ya watoto. Tushirikiane na vyombo vyetu, kama madawati ya jinsia, polisi, na ustawi wa jamii, kutoa ushahidi na kuhakikisha haki inatendeka.” Alisisitiza Malenya.
Akisoma risala ya watoto, mmoja wa wawakilishi wa watoto wa Madaba alisema: “Tunashukuru Serikali kwa madawati ya ulinzi, ruzuku ya elimu, na uboreshaji wa huduma. Lakini tunaomba jamii itimize wajibu wake wa malezi. Watoto wengine wanaishi mitaani, wanabaguliwa, wanaonewa, na kunyanyaswa. Tunaomba jamii itulinde, itupende, na ituheshimu.”
Hotuba hiyo ya watoto ilibainisha pia mafanikio yaliyopatikana, kama ujenzi wa madarasa, kuongezeka kwa madawati, na uwepo wa dawati la ulinzi wa watoto shuleni, lakini ikasisitiza haja ya kuimarisha ushirikiano wa jamii.
Siku ya Mtoto wa Afrika inatufundisha kwamba watoto ni urithi wa kesho. Wakiandaliwa vyema, wataleta maendeleo, amani, na ustawi wa taifa. Hii ni fursa ya pekee kwa Serikali, jamii, wazazi na wadau wote kuungana, kupanga, na kutekeleza mikakati ya kuwalinda, kuwaendeleza na kuwatunza watoto
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.