IKIWA ni mwanzo wa mchakato wa kisiasa kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025, Makamu Mwenyekiti wa CCM Taifa, Mheshimiwa Stephen Masatu Wasira, ameibua hisia kali na kumbukumbu za kihistoria katika mkutano mkubwa wa kichama uliofanyika katika Ukumbi wa Njunde, Kijiji cha Peramiho, Wilaya ya Songea mkoani Ruvuma.
Akizungumza mbele ya umati wa wanachama, wazee wa mila, viongozi wa dini na wa jumuiya mbalimbali za CCM, Wasira alitoa wito mzito wa kuilinda amani ya Tanzania wakati huu wa maandalizi ya uchaguzi mkuu.
Katika hotuba yenye msisimko na mapokeo makubwa kutoka kwa hadhira, Wasira alikumbusha namna vyama vya TANU na ASP vilivyoshika hatamu katika kupigania uhuru wa Tanganyika na Zanzibar, kabla ya kuungana mwaka 1977 kuunda Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Alisisitiza kuwa CCM si chama tu cha siasa, bali ni taasisi yenye mizizi ya ukombozi barani Afrika, na mchango wake umeifanya Tanzania kuwa nchi inayoheshimika duniani kwa kudumisha amani, mshikamano na maridhiano ya kitaifa.
“Amani tunayojivunia si bahati nasibu, bali ni zao la umoja, uvumilivu na uongozi wa busara uliowekwa na waasisi wetu. Sasa ni zamu yetu kuhakikisha tunairithisha vizazi vijavyo,” alisema Wasira huku akishangiliwa na umati.
Katika kuhamasisha mshikamano kuelekea uchaguzi, Wasira alisisitiza umuhimu wa wananchi kushiriki katika michakato ya kisiasa kwa njia ya kistaarabu na kuepuka lugha au matendo ya kuchochea migogoro. Alisema kuwa uchaguzi si uwanja wa vita bali ni jukwaa la demokrasia ambapo kila Mtanzania anapaswa kutumia uhuru wake kwa hekima na kwa ajili ya kuijenga nchi.
Akihitimisha, Wasira alitoa ujumbe mzito: “Tanzania ni mfano wa kuigwa barani Afrika kwa kuwa kisiwa cha amani. Tuitunze. Tuilinde. Tusiruhusu chokochoko za kisiasa kuigawa nchi yetu. Tunaposhiriki uchaguzi, tushiriki kama wamoja, si maadui.”
Ziara ya Mheshimiwa Wasira si tu ilihimiza uhai wa chama kuelekea uchaguzi, bali pia imeibua mjadala mpana kuhusu wajibu wa kila raia katika kulinda amani ya taifa. Katika kipindi hiki cha maandalizi ya uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025 ujumbe wake unabeba uzito mkubwa: Tanzania ni yetu sote, tuitunze kwa busara, kwa mshikamano, na kwa moyo wa kizalendo.