Wakulima wa kijiji cha Mcheshi, Tarafa ya Lukumbule, Wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma wamevuna neema katika mnada wa kwanza wa zao la ufuta msimu huu, ambapo tani 1,273.487 zenye thamani ya Shilingi bilioni 3.1 ziliuzwa kupitia Chama cha Msingi cha Ushirika cha Mruji Amcos.
Meneja Mkuu wa Chama Kikuu cha Ushirika Tunduru (TAMCU), Marcelino Mrope, alisema bei ya chini ilikuwa Shilingi 2,410 kwa kilo, ya juu Shilingi 2,460, huku wastani ukiwa Shilingi 2,439—bei ambayo ni pungufu kidogo ikilinganishwa na msimu uliopita.
Mkuu wa Wilaya ya Tunduru, Mheshimiwa Simon Chacha, alieleza kuwa mafanikio hayo ni matokeo ya mazingira bora ya soko yaliyowekwa na Serikali kupitia Wizara ya Kilimo.
Amesisitiza kuwa mfumo wa stakabadhi ghalani utaendelea kuimarishwa ili kuwahakikishia wakulima masoko ya uhakika na bei nzuri.
Alitoa wito kwa wakulima kutumia taasisi za kifedha kupokea malipo yao badala ya kubeba fedha taslimu, huku akiwahimiza kutumia mapato kuboresha maisha yao badala ya kuzitumia kwa anasa.
Kwa upande wake, Kaimu Afisa Kilimo wa Wilaya ya Tunduru, Gallus Makwisa, alieleza kuwa wakulima wa Tunduru wamevuka lengo kwa mara ya pili mfululizo kwa kuzalisha tani 8,000 mwaka 2024 kutoka tani 4,000 mwaka 2023.
Halmashauri kwa kushirikiana na Serikali ya Mkoa wa Ruvuma imesambaza tani 8,000 za mbegu bora katika kata 36, lengo likiwa ni kuongeza tija na ubora wa ufuta unaokidhi ushindani wa soko la ndani na nje ya nchi.
Afisa Masoko wa TAMCU, Stella Msengi, alieleza kuwa msimu wa 2024/2025 umevuka matarajio kwa kukusanya kilo 8,774,621 za ufuta, sawa na ongezeko la asilimia 60.09 ikilinganishwa na msimu uliopita.
Alisema matarajio kwa msimu wa 2025/2026 ni kukusanya kilo 12,811,100, huku akiwahamasisha wakulima kuendelea kushirikiana na vyama vya msingi ili kunufaika na mfumo wa mnada unaowaletea tija kubwa.
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.