Wakulima wa mahindi mkoani Ruvuma wamesisitiza ombi lao kwa Serikali kufungua soko la mahindi haraka, ili waepuke hasara inayoweza kuwakumba kutokana na bei duni inayotolewa na wafanyabiashara wa mitaani.
Wamesema Serikali, kupitia Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA), ndiyo mkombozi wa pekee wa wakulima, kwani hununua mahindi kwa bei nzuri kati ya Shilingi 500 hadi 700 kwa kilo ikilinganishwa na wafanyabiashara binafsi wanaotoa Shilingi 300 hadi 400 tu, bei inayowadidimiza kiuchumi.
John Nchimbi, mkulima wa kijiji cha Matiri, Wilayani Mbinga, alisema kuchelewa kufunguliwa soko la NFRA kunawaumiza, kwani wafanyabiashara wa mitaani wameshaanza kuwanunulia mahindi shambani kwa bei ya hasara.
“Tunaiomba Serikali ifungue soko haraka ili tusipate hasara, wafanyabiashara wanazunguka mashambani na kununua kwa bei ya chini. Hii si haki kwetu,” alisema Nchimbi.
Erasto Mapunda wa Magagura, aliongeza kuwa ucheleweshaji wa soko una athari si tu kiuchumi, lakini pia kiafya na kimaisha, kwani familia nyingi zinategemea mahindi kama kitega uchumi.
Naye Sebastian Komba wa Lukarasi, aliitaka NFRA kuzingatia jiografia ya Wilaya ya Mbinga, hususan kata nane zinazozalisha mahindi kwa wingi, kama Mkako, Kigonsera, Amanimakolo, Namswea, Muungano, Matiri, Lukarasi, na Ruanda.
Amesema kuwa Kituo cha Kigonsera pekee hakiwezi kuhudumia wakulima wote, kwani umbali wa kusafirisha ni mrefu, na gharama zinawakandamiza.
Takwimu za NFRA kanda ya Songea zinaonesha kwamba, kwa mwaka wa fedha 2024/2025, lengo la ununuzi wa mahindi lilikuwa tani 72,000, lakini hadi Desemba 2024, NFRA ilinunua tani 118,292, sawa na asilimia 164.3 ya lengo, na akiba ya mahindi ilifikia tani 196,498,737.
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.