Katibu Tawala wa Mkoa wa Ruvuma, Bi. Mary Makondo, amesema kuwa juhudi za Halmashauri ya Wilaya ya Nyasa katika kushughulikia hoja na mapendekezo ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) ni za kuridhisha kwa kiasi fulani kwa kuwa bado jitihada zinahitajika katika kutekeleza hoja hizo.
Makondo ametoa kauli hiyo wakati akisoma hotuba kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Kanali Ahmed Abbas Ahmed, katika Baraza Maalum la kujadili hoja za CAG lililofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa halmashauri hiyo.
"Pamoja na kupata hati safi, mwenendo wenu wa ushughulikiaji wa hoja na mapendekezo ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali pamoja na maagizo ya LAAC kwa kiasi fulani unaridhisha, namaanisha bado zipo jitihada ambazo mnapaswa kuzifanyia kazi ili tuweze kufikia hatua nyingine ya kuzimaliza hoja pamoja na maelekezo ya kamati," alisema Makondo.
Amebainisha kuwa kwa mujibu wa ripoti ya CAG kwa mwaka wa fedha ulioishia Juni 30, 2024, jumla ya hoja 41 zilitolewa kwa Halmashauri ya Nyasa, kati ya hizo, hoja 24 zimefanyiwa kazi na kufungwa, 17 zipo katika hatua mbalimbali za utekelezaji, pia bado kuna hoja 12 za miaka iliyopita na maagizo matano ya Kamati ya Bunge ya LAAC ambayo hayajatekelezwa ipasavyo.
Makondo amewaagiza wakuu wa idara na vitengo vya halmashauri kushiriki kikamilifu katika kuandaa majibu ya hoja pamoja na mpango kazi wa utekelezaji hoja za CAG, kuandaa taarifa za hesabu za mwisho wa mwaka kwa kuzingatia viwango vya kimataifa vya uhasibu katika sekta ya umma, huku akisisitiza kuchukua hatua za kinidhamu dhidi ya watumishi watakaobainika kusababisha hoja au hasara kutokana na uzembe.
Kwa upande wake, Katibu Tawala wa Wilaya ya Nyasa, Bw. Salum Ismail, akimwakilisha Mkuu wa Wilaya Mhe. Peres Magiri, amewapongeza madiwani na menejimenti ya halmashauri, ikiongozwa na Mkurugenzi Mtendaji kwa kazi nzuri iliyowezesha halmashauri kupata hati safi.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Nyasa Bw. Khalid Khalif ameahidi kuwa Halmashauri ya Nyasa itaendelea kutekeleza majukumu ya serikali kwa kuzingatia sera, sheria, kanuni, taratibu na miongozo kwa uadilifu na uwajibikaji wa hali ya juu.
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.