Wakulima wa zao la kahawa katika kijiji cha Mpepo, Wilaya ya Nyasa mkoani Ruvuma wamefurahia mafanikio makubwa yaliyotokana na msaada wa mbolea ya ruzuku inayotolewa na Serikali. Mbolea hiyo imeleta mapinduzi makubwa kwenye kilimo cha kahawa kwa kuongeza uzalishaji na kupunguza gharama za uzalishaji, huku pia ikiongeza ajira kwa vijana na wanawake kupitia kuongezeka kwa mahitaji ya nguvu kazi mashambani.
Ilbert Mahai, mkulima mwenye shamba la ekari 19 katika kijiji cha Mpepo, amesema amepata mafanikio makubwa baada ya kuanza kutumia mbolea ya ruzuku. Ameongeza uzalishaji kutoka tani 20 msimu wa 2022/2023 hadi zaidi ya tani 150 msimu wa 2024/2025. Mahai anatarajia kuvuna tani 200 katika msimu ujao kutokana na maandalizi ya mapema yaliyowezeshwa na upatikanaji wa mbegu na pembejeo kupitia Chama cha Ushirika Mapendo.
Kwa upande wake, Alto Matembo kutoka kijiji cha Ndondo amesema zao la kahawa limemwezesha kujenga nyumba bora na kuwasomesha watoto hadi chuo kikuu. Amewashauri vijana wa Nyasa wajikite kwenye kilimo cha kahawa ambacho kwa sasa kina tija kubwa baada ya bei kupanda kutoka Sh.4,500 hadi Sh.10,000 kwa kilo moja. Aidha, ameihimiza Serikali kuendelea kutoa pembejeo kwa wakati na kudhibiti gharama za usafirishaji wa pembejeo hizo.
Mkulima Method Ngonyani kutoka Mtetema ameipongeza Serikali kwa kuanzisha mradi wa miche bora ya kahawa ya aina ya Kombat, ambayo inasambazwa bure kupitia Halmashauri na Bodi ya Kahawa Tanzania. Mradi huo umewasaidia wakulima wengi kuachana na mazao yasiyo na faida kama mahindi na maharage, na kuelekeza nguvu zao kwenye kahawa yenye tija zaidi.
Katibu wa Chama cha Msingi cha Ushirika Mapendo, Panglas Komba amesema wamefanikiwa kununua mtambo wa kuchakata kahawa unaohudumia wakulima 200 kwa wakati mmoja. Hata hivyo, amesema changamoto ni uwezo mdogo wa mtambo huo ukilinganisha na mahitaji makubwa ya wakulima. Ameiomba Serikali kuwasaidia mashine yenye uwezo mkubwa zaidi ili kuongeza ubora na wingi wa kahawa itakayowahi soko la minada kwa bei nzuri.
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.