Katika hatua ya kuhamasisha uelewa wa masuala ya kifedha kwa wananchi wa vijijini, Benki ya NMB imeendesha mafunzo kabambe ya elimu ya kifedha kwa zaidi ya vikundi 50 katika kata ya Peramiho, Halmashauri ya Songea Vijijini mkoani Ruvuma.
Mafunzo hayo yalilenga kuwajengea uwezo viongozi wa vikundi vya kijamii ili waweze kusimamia vizuri fedha, kuweka akiba na kutumia huduma za kibenki kwa tija.
Tukio hilo lililovuta mamia ya wananchi wa Peramiho, lilichangamka zaidi kwa michezo ya ukakamavu iliyoambatana na mafunzo hayo ikiwemo kuvuta kamba, mbio za magunia, netiboli na mpira wa miguu.
Michezo hiyo ililenga kuimarisha mshikamano wa kijamii, kuhamasisha ushiriki wa vikundi na kutoa ujumbe wa mshikamano katika maendeleo ya kiuchumi.
Akizungumza kwenye mafunzo hayo,Kaimu Meneja wa NMB Kanda ya Kusini, Roman Degeleki, alieleza kuwa benki hiyo imejipambanua kwa kuwafikia Watanzania wote hadi ngazi za vijiji.
“NMB ni benki inayowafuata wateja popote walipo. Tuna mawakala zaidi ya 7,000 nchini ambao wanahakikisha huduma zetu zinapatikana hata sehemu zisizofikika kirahisi,” alisema kwa msisitizo.
Naye Afisa Mahusiano wa NMB Tawi la Masasi, Fanueli Duya, alitoa shukrani kwa wateja wa benki hiyo na kuwataka kutumia fursa ya kufungua akaunti mpya kupitia kampeni yao endelevu ya “Fungua Akaunti, Jenga Maisha Yako.”
Alibainisha kuwa huduma hiyo inalenga kuongeza ujumuishwaji wa wananchi katika mfumo rasmi wa kifedha.
Hatua ya NMB kutoa mafunzo haya inathibitisha dhamira ya kweli ya benki hiyo katika kuinua maisha ya wananchi kwa vitendo.
Kwa kuwajengea uwezo viongozi wa vikundi mashinani, NMB inachochea maendeleo ya kiuchumi, inaimarisha elimu ya kifedha na kuleta mapinduzi ya kibenki vijijini.
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.