Katibu Tawala wa Mkoa wa Ruvuma, Bi. Mary Makondo, amesema katika mkoa wa Ruvuma takwimu za ukusanyaji wa damu zimeonyesha kuwa na mafanikio na kuongezeka mwaka hadi mwaka.
Ameyasema hayo wakati akifungua kikao cha maandalizi kuelekea kilele cha wiki ya uchangiaji wa hiari wa Damu Salama ambacho hufanyika Juni 14 kila mwaka, kikao hicho kimefanyika katika ukumbi wa Manispaa ya Songea.
"Mwaka 2022 chupa za damu zilikusanywa 3,600 sawa na asilimia 24.5 ya mahitaji, zilifanyiwa vipimo maabara na kusambazwa, idadi hii imeongezeka hadi kufikia chupa 12,278 sawa na asilimia 83 ya mahitaji kwa mwaka 2023, kufikia chupa 7,016 sawa na asilimia 47.4 ya mahitaji ya mkoa kwa mwaka 2024, katika kipindi cha Januari hadi Mei 2025 Mkoa umekusanya chupa 2,952 sawa na asilimia 20 ya lengo la mwaka yaani chupa 14,789 bado haujakidhi mahitaji," alisema Makondo.
Ameeleza kuwa ili kukabiliana na hali hiyo Serikali imeimarisha upatikanaji wa huduma za damu salama kwa kununua majokofu, amesema mkoa una vituo 37 ambavyo vinatoa huduma ya Damu Salama, vituo 26 sawa na asilimia 70 vinamilikiwa na Serikali wakati vituo 11 sawa na asilimia 30 vinamilikiwa na taasisi za dini (FBO).
Makondo amebainisha kuwa watumiaji wakubwa wa damu ni watoto walio chini ya miaka mitano ambao wanatumia damu inayokusanywa kwa asilimia 50, mama wajawazito ambao hupoteza damu nyingi wakati wa kujifungua wanatumia asilimia 30 ya damu inayokusanywa, lakini wahanga wa ajali, wagonjwa wa magonjwa ya ndani na wanaopata tiba kwa njia ya upasuaji ambao wakati mwingine hupoteza damu wote kwa pamoja wanatumia asilimia 20 ya damu inayokusanywa.
Kwa upande wake Mganga Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Dr. Louis Chomboko, amesema bado kuna uhitaji mkubwa wa damu kutokana na changamoto mbalimbali zinazojitokeza katika jamii zikiwepo ajali za barabarani.
Ametoa wito kwa wananchi katika Halmashauri zote za mkoa wa Ruvuma kujitokeza kuchangia damu ili kuokoa maisha ya wahitaji wa damu salama, akisisitiza zoezi hilo kwa mwaka huu 2025 tayari limeanza Juni 1 na linatarajiwa kumalizika Juni 14.
Wiki ya Uchangiaji wa Hiari wa Damu Salama hufanyika kila mwaka duniani kote kuanzia Juni 1 hadi 14, ikiwa na lengo la kuhamasisha uchangiaji wa damu kwa hiari ili kuokoa maisha ya wenye uhitaji. Kauli mbiu ya mwaka huu inasema: 'Changia Damu, Leta Matumaini; Pamoja Tunaokoa Maisha.'
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.