Wakazi wa Mkoa wa Ruvuma wamepata neema kubwa ya huduma bora za afya baada ya kuzinduliwa rasmi kwa kambi ya madaktari bingwa na bingwa bobezi 57 kupitia mpango wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Uzinduzi huo umefanyika katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, ukiongozwa na Katibu Tawala wa Mkoa, Bi. Mary Makondo kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa, Kanali Ahmed Abbas Ahmed.
Bi. Makondo amesema kuwa huduma hizo zitatolewa kwa gharama nafuu kwa muda wa siku sita kuanzia Mei 26 hadi 31, 2025, katika hospitali zote za halmashauri ndani ya mkoa wa Ruvuma.
“Kila hospitali ya halmashauri itapokea seti ya madaktari bingwa sita na muuguzi bingwa mmoja,” amesema Makondo.
“Wataalamu hao watahusisha ubingwa wa magonjwa ya wanawake na ukunga,bingwa bobezi wa magonjwa ya watoto na watoto wachanga,bingwa wa upasuaji na mfumo wa mkojo, bingwa wa usingizi na ganzi, bingwa wa magonjwa ya ndani, bingwa wa kinywa na meno, bingwa wa masikio, pua na koo na muuguzi bobezi.”
Ameeleza kuwa utekelezaji wa huduma hizo unategemea mazingira bora yaliyowekwa na serikali ikiwemo upatikanaji wa dawa, vifaa tiba, na miundombinu ya kisasa ya huduma za afya.
Aidha, Bi. Makondo amesisitiza kuwa serikali inaendelea kuboresha sekta ya afya kwa kasi kubwa, ikijumuisha ujenzi na ukamilishaji wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa, hospitali za halmashauri, vituo vya afya, zahanati na majengo ya huduma za dharura.
Ametoa rai kwa viongozi wa wilaya, halmashauri, wabunge, na madiwani kuhakikisha wanatoa ushirikiano wa kutosha kwa kuhamasisha wananchi kuhudhuria na kunufaika na huduma hizo za kibingwa.
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.