Katibu Tawala wa Mkoa wa Ruvuma, Bi. Mary Makondo, amezindua awamu ya tatu ya kambi ya madaktari bingwa na bingwa bobezi wa Dkt. Samia katika mkoa wa Ruvuma.
Akifungua kambi hiyo ya siku sita itakayoanza tarehe 26 hadi 31 Mei 2025, kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Makondo amesema, ujio wa madaktari hao unasogeza huduma karibu zaidi na wananchi hivyo anatarajia kuwa huduma zitakazotolewa zitakuwa kamilifu.
“Serikali yetu imeboresha upatikanaji wa dawa, vifaa tiba pamoja na miundombinu ya kutolea huduma za afya, kwa hiyo ni matumaini yangu kuwa huduma zitakazotolewa zitakuwa kamilifu,” alisema Makondo.
Akitoa Salamu za Wizara, Afisa wa Idara ya Afya ya Uzazi, Mama na Mtoto, Bi. Grace Maliki, amesema huduma hizo za madaktari bingwa wa Dkt. Samia zinaletwa karibu na wananchi kwa gharama nafuu ili kuwapunguzia adha ya kufuata huduma hizo mbali na maeneo wanayoishi.
Ametoa wito kwa madaktari hao bingwa na bingwa bobezi kuhakikisha wanawajengea uwezo wataalam wengine ambao watawakuta kwenye maeneo wanayoenda kutoa huduma za kibingwa ikiwa lengo ni kuhakikisha kuwa wataalam hao wanapata ujuzi wa ziada ili kuendelea kutoa huduma bora kwa wananchi hata baada ya kambi hiyo kumalizika.
Naye Mganga Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Dr. Louis Chomboko, amesema moja kati ya mikakati ya serikali ya awamu ya sita ni kuhakikisha wananchi wanakuwa na afya njema ili washiriki kikamilifu katika ustawi wa nchi kwa kuwa wananchi wenye afya ndio wenye tija katika kuzalisha na ustawi wa nchi.
Amebainisha kuwa katika kila hospitali ya halmashauri huduma za kibingwa zitakazotolewa ni za magonjwa ya wanawake na ukunga, watoto na watoto wachanga, upasuaji na mfumo wa mkojo, usingizi na ganzi, magonjwa ya ndani, kinywa na meno wakati huo daktari bingwa wa mifupa atakuwa Songea DC na daktari bingwa wa masikio, pua na koo atakuwa Mbinga TC.
Katibu wa CCM Songea Mjini, James Mgego, akimwakilisha mwenyekiti wa CCM mkoa wa Ruvuma, ameeleza kuwa ujio wa madaktari bingwa katika awamu zilizopita umekuwa na mafanikio makubwa katika kutoa huduma za afya kwa wananchi akisisitiza kuwa chama kina imani kwamba hata awamu hii ya tatu italeta matokeo chanya katika kutoa huduma hizo.
Awamu ya pili ya huduma za kibingwa na ubingwa bobezi iliyofanyika kuanzia Oktoba 10 hadi Novemba 03, 2024 katika mkoa wa Ruvuma, wagonjwa 10,819 walihudumiwa na watoa huduma 334 wa fani mbalimali walijengewa uwezo.
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.