Uzalishaji wa mazao ya biashara katika Mkoa wa Ruvuma umefikia hatua ya juu ya kihistoria, baada ya zao la tumbaku kufikia tani 2,053 kwa msimu wa 2024/2025, kutoka tani 1,664 msimu uliopita.
Ongezeko hilo limeashiria kurudi kwa nguvu kwa wakulima katika sekta ya kilimo cha biashara, huku wakinufaika na mifumo rafiki ya masoko na ongezeko la bei katika soko la dunia.
Kwa upande wa zao la ufuta, hali ni ya matumaini makubwa zaidi baada ya kufikia tani 5,538 katika msimu huu, huku matarajio yakiwa ni kuvuna hadi tani 10,000 msimu ujao wa 2025/2026.
Ongezeko hilo limechochewa na utekelezaji madhubuti wa mfumo wa stakabadhi ghalani na juhudi za vyama vya ushirika kuratibu masoko kwa ufanisi.
Akizungumza katika Mkutano Mkuu wa 22 wa Chama Kikuu cha Ushirika wa Mazao Songea Namtumbo (SONAMCU) uliofanyika mjini Songea, Katibu Tawala wa Mkoa wa Ruvuma, Mary Makondo, amesema mafanikio hayo yanadhihirisha mchango mkubwa wa ushirika katika kuinua kipato cha wakulima na uchumi wa mkoa.
Ameipongeza SONAMCU kwa kuwa nguzo muhimu katika uendeshaji wa masoko ya mazao na kuwahakikishia wakulima maslahi yao.
Katika hatua nyingine muhimu, Makondo ametangaza kuwa msimu mpya wa minada ya ufuta utaanza rasmi Mei 29, 2025 katika Wilaya ya Namtumbo, akiwataka wakulima kujitokeza kwa wingi ili kufaidika na bei nzuri zinazopatikana kupitia mfumo rasmi wa minada unaolenga kuwapatia tija kubwa zaidi.
Kwa upande wake, Meneja wa SONAMCU, Juma Mwanga, ameeleza kuwa chama hicho kimejipanga kikamilifu kuratibu masoko ya mazao ya biashara kama tumbaku, mbaazi na ufuta kupitia mfumo wa stakabadhi ghalani, ambao umeongeza uwazi, usalama wa mauzo, na mapato kwa wakulima wa Mkoa wa Ruvuma.
Kuimarika kwa uzalishaji wa mazao ya biashara mkoani Ruvuma ni ushahidi wa mafanikio ya sera za ushirika na mifumo ya kisasa ya masoko.
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.