Serikali kupitia Wizara ya Nishati imeanza rasmi zoezi la ulipaji wa fidia kwa wananchi waliopisha mradi mkubwa wa kusambaza umeme wa gridi ya taifa wenye nguvu ya kilovoti 220 kutoka Songea hadi Tunduru mkoani Ruvuma. Mradi huo wa kimkakati unaotarajiwa kuongeza upatikanaji wa nishati ya umeme vijijini na mijini, unatarajiwa kujengwa kwa urefu wa kilometa 264 ambapo takribani shilingi bilioni 2.5 zinatolewa kwa wakazi walioguswa.
Zoezi hilo limezinduliwa katika mtaa wa Mletele, Manispaa ya Songea ambapo zaidi ya wananchi 200 wameanza kulipwa fidia. Akizungumza wakati wa zoezi hilo, Afisa Tarafa wa Songea Mashariki, Dismas Komba amewataka wananchi waliopokea fidia kupisha mara moja maeneo yao ili serikali iendelee na ujenzi wa miundombinu ya umeme bila kuchelewa zaidi. “Ukishalipwa, toa mazao yako kama mahindi ambayo yameshaiva, usichukue muda mrefu. Tunaomba usaidie taifa kwa kuacha eneo bila usumbufu,” amesema Komba.
Afisa huyo pia aliwataka wananchi kutotumia fedha hizo vibaya kwa sababu ni sehemu ya mchango wao katika maendeleo ya nchi. “Msije mkazivunja ndoa zenu kwa sababu ya fidia, hizi fedha ni kwa ajili ya kupisha maendeleo. Nawaamini kuwa nyie ni watu wa kuelewa,” amesisitiza huku akipongeza ushirikiano kutoka kwa wananchi waliokwishalipwa.
Kwa upande wake, Meneja Mawasiliano wa TANESCO mkoani Ruvuma, Aran Njilo, amewataka wananchi wanaoishi jirani na maeneo ya mradi kushirikiana kikamilifu na mkandarasi pamoja na kuhakikisha miundombinu ya umeme inalindwa dhidi ya wizi na uharibifu. “Tunaomba wananchi mtambue huu ni mradi wa maendeleo. Mkandarasi ataendelea na kazi, hivyo ni muhimu tushirikiane na kulinda vifaa na miundombinu ili mradi huu uwe na tija inayotarajiwa,” amesema Njilo.
Mradi wa kusafirisha umeme wa Songea-Tunduru ni sehemu ya jitihada za serikali kupitia TANESCO kupanua mtandao wa umeme wa gridi ya taifa kuelekea Kusini mwa Tanzania. Kukamilika kwake kunatarajiwa kuondoa changamoto ya umeme katika wilaya ya Tunduru na kuchochea ukuaji wa uchumi kupitia sekta za viwanda, biashara na huduma.
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.