Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Ruvuma imefanikiwa kuwezesha upatikanaji wa fedha za makusanyo ya Halmashauri ya Wilaya ya Songea.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo na Naibu Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Ruvuma, Janeth F. Haule, mafanikio hayo yamepatikana kupitia utekelezaji wa majukumu ya taasisi hiyo kwa kipindi cha Januari hadi Machi 2025.
Imeelezwa kuwa jumla ya Shilingi 9,205,158.44 zilizotokana na makusanyo ya mapato kutoka vyanzo mbalimbali vilivyokusanywa na mawakala kwa njia ya mifumo ya kielektroniki, hazikuwasilishwa benki kama taratibu zinavyotaka. Hata hivyo, baada ya TAKUKURU kufanya ufuatiliaji wa karibu, fedha hizo hatimaye ziliwasilishwa benki.
Aidha, ufuatiliaji huo umechochea ongezeko la makusanyo ya mapato katika Halmashauri hiyo, hususan kwenye Divisheni za Kilimo, Mifugo na Uvuvi; Biashara; Ardhi na Maliasili, ambapo kiwango cha makusanyo kimepanda kutoka asilimia 50 hadi kufikia asilimia 102 kupitia mifumo ya kielektroniki.
TAKUKURU imetoa ushauri wa marekebisho kwenye miradi mitatu (3) ya sekta za Miundombinu, Kilimo na Fedha, yenye jumla ya thamani ya Shilingi 29,917,135,361.43, baada ya kubaini mapungufu katika utekelezaji wake.
Katika kipindi hicho cha Januari – Machi 2025, TAKUKURU Mkoa wa Ruvuma imefanya chambuzi tatu (3) na kuendesha warsha tatu (3) na wadau mbalimbali, ambazo zimesababisha kufikiwa kwa maazimio 16 ya kuziba mianya ya rushwa. Programu hizi zinatekelezwa katika kata 12, ambapo jumla ya kero 118 zilibainika, kati ya hizo kero 89 zimetatuliwa na kero 29 zinaendelea kushughulikiwa.
Aidha TAKUKURU imefanya Semina 24, Uimarishaji wa klabu za wapinga rushwa 53, Mikutano ya hadhara 26, Maonesho 06, Makala 02 na Vipindi vya Redio 03 ikiwa pamoja na Malalamiko 100 yalipokelewa, Kati ya hayo, 80 yalihusu rushwa na 20 hayakuhusu rushwa huku Kesi 04 zilifunguliwa Mahakamani ambapo kesi 03 zimetolewa Hukumu na Jamhuri imeshinda kesi zote 03 na hakuna kesi iliyoshindwa.
Akihitimisha taarifa yake, Janeth Haule ametoa wito kwa wananchi kujitayarisha na kushiriki kikamilifu kwenye Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025 kwa kuepuka vitendo vya rushwa ili kuhakikisha taifa linapata viongozi waadilifu, watakaowezesha maendeleo na kudumisha amani nchini
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.