Katika kipindi cha miaka minne tu, Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeiweka Ruvuma katika ramani ya maendeleo kupitia uwekezaji wa kihistoria wa zaidi ya shilingi trilioni 1.18, ukigusa kila kona ya maisha ya wananchi kutoka elimu hadi afya, kutoka barabara hadi nishati, kutoka maji hadi kilimo.
Elimu ya Kisasa kwa Watoto wa Ruvuma
Kwa macho ya wengi, mabadiliko haya yameonekana dhahiri katika sekta ya elimu. Serikali imetumia shilingi bilioni 192.3 kubadilisha uso wa elimu mkoani hapa.
Vyumba vya madarasa 1,717 vimejengwa, shule mpya 67 zimeanzishwa, mabweni 95, maabara 98 na nyumba za walimu 106 zimejengwa kwa kiwango cha kisasa.
Hakuna mzazi anayelazimika tena kuchanga hela ya madawati wala kujenga darasa. Elimu bila ada si tu kauli, bali ni uhalisia. Hali hii imeongeza mahudhurio ya wanafunzi, hususan wa kike, ambao sasa wanasoma katika mazingira bora na salama.
Afya: Mgonjwa Hasafirishwi Tena kwa Baiskeli
Katika nyanja ya afya, bilioni 45.3 zimetumika kujenga vituo vya afya 16, hospitali za wilaya tano, zahanati 47 na Hospitali ya Rufaa ya Mkoa yenye huduma za kisasa kama vile majengo ya dharura (EMD).
Vifaa tiba vya kisasa, magari 21 ya kubeba wagonjwa, na magari maalum ya kusambaza chanjo vimeongeza ufanisi mkubwa.
Mama Salome Komba wa Kindimbachini Wilayani Mbinga analia kwa furaha: "Niliweza kujifungua salama katika kituo cha afya Kindimbachini kilichojengwa na serikali; zamani tulitembea hadi Peramiho "
Barabara Zamfungulia Mkulima Soko
Miundombinu ya barabara imepokea mwelekeo mpya. Kwa kutumia shilingi bilioni 301.2, Serikali imejenga barabara ya lami ya Mbinga-Mbambabay yenye urefu wa 66KM, barabara zingine za lami 141.75KM, na madaraja marefu yenye urefu wa 231.5M.
Barabara hizi si tu zimeunganisha wilaya, bali zimefungua masoko kwa wakulima, wafanyabiashara na wanafunzi. Ni maendeleo yanayoonekana kwa macho.
Umeme: Mwanga Waingia Kila Kijiji
Ndoto ya kila kijiji kuwa na umeme sasa ni historia. Kwa uwekezaji wa shilingi bilioni 168.7, vijiji vyote 554 vya Ruvuma vimeunganishwa na gridi ya taifa. Migodi midogo, mashine za kusaga, na shughuli za viwanda vidogo zimeshika kasi.
Kijiji cha Lundo wilayani Nyasa kilichokuwa gizani kwa miaka mingi sasa kinang'ara. "Siku hizi tunatazama TV na watoto wanajisomea hadi usiku," anasema Bi Frida Ligola kwa furaha.
Maji: Kinamama Hawabebi Tena Ndoo Kilomita Nne
Maji safi na salama sasa ni haki, si fadhila. Serikali imetumia bilioni 228.92 kuboresha huduma hii muhimu. Mradi mkubwa wa maji wa bilioni 145 katika Mji wa Songea na umeleta nuru inatakayomaliza maji ya mgawo katika mji huo.
Wanawake wanajivunia muda zaidi wa kufanya shughuli za uzalishaji badala ya kutumia saa kadhaa kutafuta maji.
Usafiri na usafirishaji Waongeza Kasi
Kwa kutumia bilioni 141, Serikali imekarabati Uwanja wa Ndege wa Songea na kujenga bandari za kisasa Ndumbi na Mbamba-bay. Vituo vya mabasi vya kisasa vinajengwa, na haya yote yanaifanya Ruvuma kuwa lango la biashara Kusini mwa Tanzania.
Kilimo na Ushirika vinavyowanufaisha wakulima
Sekta ya kilimo haijatelekezwa. Zaidi ya bilioni 96.8 zimetumika katika kujenga maghala 28, kusambaza tani 118,292 za mahindi, na pembejeo. Maafisa ugani 281 wamepewa pikipiki na nyumba mpya tano zimejengwa kwao.
Kilimo kimegeuka kuwa cha kisasa. Mkulima si mtumwa tena, ni mjasiriamali anayejua thamani ya mazao yake.
Mifugo na Uvuvi: Samaki na Maziwa Zaidi
Katika sekta ya mifugo na uvuvi, bilioni 2.228 zimetumika kuanzisha mashamba darasa 8, chanjo kwa mifugo, dawa za kuogeshea, boti za kisasa, soko la samaki na mwalo mpya.
Zaidi ya vifaranga 50,000 vya samaki wamesambazwa kuongeza uzalishaji na pato la wananchi waishio kando ya Ziwa Nyasa.
Uongozi na Utawala: Serikali Karibu na Wananchi
Kwa kutumia bilioni 9.5, nyumba za viongozi zimeboreshwa, majengo ya ofisi yamejengwa, pikipiki 281 zimetolewa kwa watendaji wa kata, na mahakama mpya zimejengwa.
Hii imeboresha upatikanaji wa haki na uwajibikaji wa watumishi wa umma kwa wananch
Maendeleo ya Mkoa wa Ruvuma si ndoto tena. Ni mabadiliko yanayoshikika, yanayoishi, na yanayoleta tumaini jipya kwa maelfu ya wananchi waliokuwa wamesahaulika kwa miaka mingi.
Rais Samia ameandika historia Ruvuma, na historia hiyo imechorwa kwenye kila darasa jipya, kila kisima cha maji, kila barabara ya lami, na kila nyumba ya mwalimu inayong’aa chini ya jua la Kusini.
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.