Ndoto ya muda mrefu ya wananchi wa Wilaya ya Songea mkoani Ruvuma kuona barabara ya kisasa inayowaunganisha na dunia ya biashara na maendeleo hatimaye inakaribia kutimia, huku wakihakikishiwa fidia ya haki kabla ya kuanza kwa ujenzi mkubwa wa barabara ya kimkakati ya Likuyufusi–Mkayukayu yenye urefu wa kilomita 60.
Ni mradi unaogharimu Shilingi Bilioni 110.77, na unaanza rasmi wakati wowote kwa hatua ya kwanza hii ishara ya mapinduzi ya kiuchumi kwa wakazi wa mikoa ya kusini.
Katika kijiji cha Litapwasi wilayani Songea, vilio vya furaha vilisikika wakati Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) Mkoa wa Ruvuma ulipokabidhi rasmi mradi huo kwa mkandarasi kutoka kampuni ya China First Highway Engineering Co. Ltd.
Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi wa Serikali, wakiongozwa na mgeni rasmi Waziri wa Afya na Mbunge wa Jimbo la Peramiho Mheshimiwa Jenista Mhagama, Mkuu wa Wilaya ya Songea, Mhe. Kapenjama Ndile na Katibu Tawala wa Mkoa wa Ruvuma Mary Makondo ambaye alimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma,pamoja na wananchi waliokuwa na matumaini makubwa juu ya mabadiliko yanayokuja.
Kaimu Meneja wa TANROADS Mkoa wa Ruvuma, Mhandisi Fedinand Mdoe, alieleza kuwa fidia ya zaidi ya Shilingi Bilioni tano kwa wananchi 851 waliopisha ujenzi huo italipwa mapema mara baada ya fedha kupokelewa kutoka Wizara ya Fedha.
“Uthamini wa mali za wananchi tayari umekamilika. Tutahakikisha fidia inatolewa kwa haki na kwa wakati. Kamati maalum zitaanzishwa ili kushughulikia malalamiko yoyote yatakayojitokeza,” alisema Mdoe.
Kwa mujibu wa Mhandisi Mdoe, mradi huu unaojumuisha awamu ya kwanza ya ujenzi wa barabara kwa muda wa miezi 27 ikiwemo miezi mitatu ya maandalizi.
Amesisitiza kuwa kuanza kutekelezwa kwa mradi huo ni sehemu ya dhamira ya Serikali ya awamu ya sita ya Dkt. Samia Suluhu Hassan kuimarisha miundombinu katika maeneo ya kimkakati.
Baada ya awamu ya kwanza, awamu ya pili ya kilomita 64 kutoka Mkayukayu hadi eneo la Mkenda Mpaka wa Tanzania na Msumbiji inatarajiwa kuanza,sanjari na ujenzi wa madaraja ya Mitomoni na Mkenda.
Mradi huu wa barabara utaiunganisha Wilaya ya Songea na Nyasa, na pia kufungua lango la kimkakati la usafirishaji kati ya Tanzania na Msumbiji.
Akizungumza kwa msisitizo mkubwa, Mkuu wa Wilaya ya Songea, Kapenjama Ndile alisema Serikali inaendelea kuhakikisha wananchi wanapata taarifa sahihi kuhusu utekelezaji wa miradi ya maendeleo.
“Barabara hii si tu itarahisisha usafiri, bali pia itafungua fursa mpya za kiuchumi, kuongeza uwekezaji, na kubadili kabisa mwelekeo wa maendeleo ya Mkoa wa Ruvuma kwa sababu hii barabara fupi Zaidi kuelekea nchini Afrika ya Kusini,” alisema Ndile.
Katibu Tawala wa Mkoa wa Ruvuma Mary Makondo akitoa salamu za Mkoa kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa alisema serikali ya Awamu ya Sita tayari imetoa shilingi trilioni 1.8 kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo na kwamba kati ya fedha hizo sekta ya barabara imepokea Zaidi ya shilingi bilioni 300.
Mbunge wa Jimbo la Peramiho ambaye pia ni Waziri wa Afya, Mheshimiwa Jenista Mhagama, alibainisha kuwa mradi huu utasaidia kuimarisha usalama wa mipaka, kurahisisha uzalishaji na kukuza uchumi wa wananchi.
Alisisitiza umuhimu wa wananchi kuongeza uzalishaji wa mazao ya biashara, kilimo, mifugo na ujasiriamali ili kuendana na fursa mpya zitakazotokana na ujenzi wa barabara hiyo.
Wananchi wa Litapwasi waliiomba Serikali kuwasimamia wakandarasi kwa karibu ili kuhakikisha kazi inakamilika kwa ubora unaotakiwa na kwa muda uliopangwa.
Barabara ya Likuyufusi–Mkenda si mradi tu wa ujenzi wa miundombinu, bali ni ishara ya matumaini, maendeleo na mabadiliko chanya kwa maelfu ya wananchi wa mikoa ya kusini.
Mradi huu unakwenda kufungua ukurasa mpya wa uhusiano wa kibiashara kati ya Tanzania na Msumbiji, huku ukiwa msingi wa kuinua uchumi wa wananchi kwa njia endelevu.
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.