Mwenge wa Uhuru 2025 mkoani Ruvuma, umepitia na kuridhia jumla ya miradi 76 ya maendeleo yenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 95.
Taarifa hiyo imetolewa na Katibu Tawala wa Mkoa wa Ruvuma, Bi. Mary Gasper Makondo, aliyemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Kanali Ahmed Abbas Ahmed, wakati wa hafla ya makabidhiano ya Mwenge wa Uhuru kati ya Mkoa wa Ruvuma na Mtwara iliyofanyika katika viwanja vya Shule ya Msingi Lumesule, wilayani Nanyumbu mkoani Mtwara.
Mwenge wa Uhuru uliingia mkoani Ruvuma Mei 9 na kumaliza mbio zake Mei 16, ukipitia Halmashauri zote nane za mkoa huo kwa umbali wa kilomita 1,378.9.
Katika kipindi hicho, miradi yote 76 iliyotembelewa ilifanyiwa ukaguzi na hatimaye kupitishwa na timu ya wakimbiza mwenge kitaifa, ikiwa ni ishara ya mafanikio makubwa ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo inayogusa maisha ya wananchi moja kwa moja.
Kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Katibu Tawala wa Mkoa huo, alikiri rasmi kupokea Mwenge wa Uhuru kutoka kwa Bi. Mary Makondo na kuupongeza Mkoa wa Ruvuma kwa maandalizi mazuri na utekelezaji bora wa miradi.
Akihutubia hadhara hiyo, Bi. Makondo alieleza kuwa wananchi wa Ruvuma wamefaidika mno na mbio za mwenge wa Uhuru ambazo zimewaamsha katika kushiriki kikamilifu kwenye masuala ya maendeleo na kuwaasa kujitokeza kwa wingi katika uchaguzi mkuu 2025, sambamba na kauli mbiu ya mwaka huu isemayo "Jitokeze Kushiriki Uchaguzi Mkuu 2025 kwa Amani na Utulivu."
Aidha, Bi. Makondo alitumia fursa hiyo kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa mchango wake mkubwa katika kuleta maendeleo mkoani Ruvuma kupitia fedha za utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati.
Miradi hiyo ni pamoja na ujenzi wa barabara ya Mbinga–Mbamba Bay, upanuzi wa uwanja wa ndege wa Songea, ujenzi wa bandari ya Ndumbi (Nyasa), pamoja na upanuzi unaoendelea wa bandari ya Mbamba Bay.
Alisema kuwa miundombinu ya elimu, afya, maji na umeme pia imeimarishwa kwa kiasi kikubwa kupitia juhudi za serikali ya awamu ya sita.
Kwa upande wake, Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2025, Ndg. Ismail Ali Ussi, alisisitiza kuwa ujumbe wa mwaka huu ni wito mahsusi kwa Watanzania kutunza amani na kushiriki kikamilifu katika uchaguzi mkuu.
Alifurahishwa na ushirikiano wa wananchi wa Ruvuma na kuwapongeza kwa kujitokeza kwa wingi wakati wa mbio za mwenge wa uhuru. hizo.
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.