Mashindano ya UMITASHUMTA na UMISSETA kwa shule za msingi na sekondari katika Mkoa wa Ruvuma yamezinduliwa rasmi Mei 29 kwenye Uwanja wa Majimaji Manispaa ya Songea, yakishirikisha Halmashauri zote nane za mkoa wa Ruvuma.
Shughuli hiyo ya uzinduzi ilihudhuriwa na maelfu ya wanafunzi, walimu na viongozi wa serikali.
Akizungumza katika uzinduzi huo kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma,Katibu Tawala wa Mkoa wa Ruvuma, Mary Makondo, amesema mashindano ya mwaka huu yanaendeshwa kwa kaulimbiu isemayo: “Viongozi bora ni msingi wa maendeleo ya taaluma, sanaa na michezo. Shiriki uchaguzi mkuu kwa amani na utulivu.
Kauli hiyo inalenga kuhamasisha vijana kushiriki kikamilifu katika shughuli za michezo pamoja na kuwa mstari wa mbele katika kuchangia maendeleo ya taifa kupitia uongozi bora.
Makondo ameongeza kuwa serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imejidhatiti kukuza vipaji vya vijana kupitia sekta ya elimu.
Amesema tayari shule za sekondari za Maposeni,Chandarua na Mahanje mkoani Ruvuma zimeanza mchakato wa kuboresha viwanja vya michezo kwa kuweka miundombinu sahihi, hatua ambayo inalenga kuinua kiwango cha mashindano na maandalizi ya wanamichezo kwa ngazi ya kitaifa na kimataifa.
Katika kuhakikisha mashindano hayo yanazidi kuwa ya ushindani na tija, Makondo amezitaka Halmashauri zote kuweka bajeti maalum ya sekta ya michezo. “
“Michezo ni ajira, ni afya, na ni msingi wa kuibua viongozi wa kesho,” amesema Makondo huku akisisitiza umuhimu wa kuwekeza katika vipaji vya vijana kama njia mojawapo ya kujenga jamii bora yenye nguvu kazi imara.
Kwa upande wake Kaimu Afisa Elimu Mkoa wa Ruvuma, Anthony Luoga , amesema mashindano hayo ya siku nne yamepata mafanikio makubwa kwa kujumuisha jumla ya washiriki 688, walimu 73 na viongozi 27 kutoka halmashauri mbalimbali.
Amesema kupitia mashindano haya, mkoa unatarajia kupata wawakilishi mahiri watakaoshiriki mashindano ya kitaifa yatakayofanyika mkoani Iringa hivi karibuni.
Ameongeza kuwa mwaka huu Mkoa wa Ruvuma unalenga kuunda timu bora itakayoshiriki mashindano ya kimataifa nchini Kenya.
“Tunaamini vipaji vilivyopo Ruvuma vina uwezo wa kupeperusha vyema bendera ya Tanzania kimataifa,” amesema kwa msisitizo. .
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.