Katika uwanja wa Majimaji uliopo mjini Songea, shamrashamra na vifijo vilitawala wakati Katibu Tawala wa Mkoa wa Ruvuma, Bi. Mary Makondo, alipouzindua rasmi msimu wa mashindano ya michezo ya shule za msingi (UMITASHUMTA) na sekondari (UMISSETA) kwa mwaka 2025.
Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa, Kanali Ahmed Abbas Ahmed, Bi. Makondo aliwataka wananchi na wanafunzi kushiriki mashindano haya kwa amani na mshikamano, sambamba na kaulimbiu ya mwaka huu isemayo: "Viongozi bora ni msingi wa maendeleo ya taaluma, sanaa na michezo, shiriki uchaguzi mkuu wa mwaka 2025 kwa amani na utulivu."
Akielezea hatua madhubuti zilizochukuliwa na serikali kuimarisha sekta ya michezo, Bi. Makondo alisema kuwa shule tatu za Mkoa wa Ruvuma ambazo ni Maposeni, Chandarua na Mahanje zimeanza kuboreshwa viwanja vyake kwa kuweka vipimo sahihi vinavyokidhi viwango vya kitaifa. Alibainisha kuwa hatua hii si tu inalenga kuinua kiwango cha mashindano, bali pia inatoa fursa kwa vijana wenye vipaji kuibukia katika jukwaa la kitaifa na kimataifa kupitia maandalizi bora.
Aidha, Bi. Makondo alisisitiza kuwa serikali ya awamu ya sita imedhamiria kukuza michezo, sanaa na utamaduni kwa vitendo. Ameeleza kuwa mbali na kuboresha miundombinu ya michezo, serikali imeongeza idadi ya taasisi zitakazosaidia kukuza vipaji kupitia mitaala ya elimu ya sasa. Hatua hii inalenga kuhakikisha kuwa michezo si tu burudani bali pia nyenzo muhimu ya kujenga afya, nidhamu na ajira kwa vijana.
Katika kutambua mchango wa Mkoa wa Ruvuma katika maendeleo ya michezo nchini, Bi. Makondo alipongeza serikali kwa kutenga jumla ya shule 56 kwa ajili ya ukuzaji wa michezo, ambapo Mkoa wa Ruvuma umefaidika kwa kupata shule tatu. Hii ni ishara ya wazi kuwa Mkoa huu una nafasi muhimu katika mchango wa kitaifa kwenye sekta ya michezo na maendeleo ya vipaji.
Kwa upande wake, Kaimu Afisa Elimu Mkoa wa Ruvuma, Anthony Luoga, alifichua kuwa msimu huu Mkoa unajivunia jumla ya wanamichezo 688, walimu 73 na viongozi 27 ambao watauwakilisha mkoa katika mashindano ya kitaifa yatakayofanyika mkoani Iringa. Luoga alieleza kuwa maandalizi ya washiriki hao yamekamilika na matumaini ni makubwa kuwa Ruvuma itang'ara na kurejea na ushindi mkubwa kutoka Iringa.
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.