Mwenge wa uhuru umekamilisha ziara yake mkoani Ruvuma kwa kuangazia miradi ya wilaya ya Tunduru ambapo umeweza kuweka jiwe la msingi katika mradi mkubwa wa maji safi na salama wa Masuguru unaogharimu Zaidi ya shilingi bilioni 2.4.
Mwenge wa Uhuru mwaka 2025 umezindua , kukagua, kutembelea na kuweka mawe ya msingi katika miradi 11 yenye thamani ya shilingi Bilioni 3.2 wilayani Tunduru
Meneja wa RUWASA Wilaya ya Tunduru Mhandisi Maua Mgallah amesema mradi huo uliofikia asilimia 85 ya utekelezaji unakwenda kuwanufaisha wananchi wapatao 16,124 na kuongeza upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama katika wilaya hiyo kutoka asilimia 81.86 hadi kufikia asilimia 86.65.
Mwenge wa uhuru ukiwa wilayani Tunduru pia umeweka jiwe la msingi katika mradi wa ujenzi wa jengo la kusubiria ndugu wa wagonjwa katika hospitali ya wilaya ya Tunduru ambapo serikali imetenga Zaidi ya shilingi milioni 97 kutoka mapato ya ndani kutekeleza mradi huo.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru Chiza Marando amesema hadi sasa mradi umefikia asilimia 80 ya utekelezaji na kwamba mradi huo utawawezesha ndugu wa wagonjwa kutoa huduma mbalimbali kwa wagonjwa na kupunguza msongamano wa ndugu wa wagonjwa katika maeneo ya kutolea huduma hasa wodini.
Mwenge wa Uhuru ukiwa wilayani Tunduru pia umetembelea shamba la miti katika kijiji cha Chiwana lenye ukubwa wa hekari 8.23 ambalo limepandwa miti hekari 2,3 aina ya mitiki ambalo lina miti 1,551.
Mwenyekiti wa kijiji cha Chiwana Mohamed Chiulika amesema shamba darasa dogo hilo lilianzishwa mwaka 2021 kupitia mradi wa TASAF lengo likiwa ni kutunza mazingira kupitia upandaji miti.
Amezitaja baadhi ya faida ambazo zimepatikana hadi sasa kutokana na mradi huo ni pamoja na watu 50 kupata elimu ya upandaji miti na utunzaji wa mazingira,miti itakapokomaa kijiji kitaongeza mapato kupitia mbao na matumizi mbalimbali yanayotokana na miti hiyo yenye soko kubwa kimataifa.
Mwenge wa uhuru ukiwa wilayani Tunduru pia umetembelea mradi wa nishati safi ya kupikia katika shule ya sekondari Tunduru ambao unagharimu Zaidi ya shilingi milioni 24.
Katika sekondari ya Tunduru mwenge wa uhuru pia umepitia mradi wa ujenzi wa mabweni mawili na matundu sita ya vyoo.
Mwenge wa Uhuru ukiwa wilayani Tunduru pia umezindua mradi wa ujenzi w barabara ya nguzo sita-Muungano hadi Camp David yenye urefu wa kilometa 0.5 kwa kiwango cha lami unaotekelezwa na TARURA.
Meneja wa TARURA wilaya ya Tunduru Mhandisi Silnavus Ngonyani amesema mradi huo umegharimu Zaidi ya shilingi milioni 234.
Mwenge wa uhuru pia umepitia mradi wa ugawaji vyandarua kwa akinamama wajawazito na watoto wa miezi tisa ambapo mradi huo umegharimu Zaidi ya shilingi milioni 59 fedha ambazo zimetolewa na wahisani wa Global Fund.
Mwenge wa uhuru umekagua shughuli za lishe katika Halmashauri hiyo mradi ambao umegharimu shilingi 605,000.
Hata hivyo Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo Chiza Marando amelitaja lengo la kupunguza na kuzuia tatizo la udumavu katika kipindi cha siku 1000 za mwanzo wa maisha ya mtoto ambapo Halmashauri hiyo imetenga shilingi milioni 70 katika kutekeleza afua za lishe.
Akizungumza kwa nyakati tofauti baada ya kupitia miradi hiyo kiongozi wa mbio za mwenge wa uhuru kitaifa 2025 Ndugu Ismali Ali Ussi amewapongeza viongozi wa Halmashauri hiyo kwa kusimamia ipasavyo miradi hiyo ambayo imetekelezwa katika ubora unaolingana na thamani ya fedha.
Ussi amewakumbusha wananchi wote waliojiandikisha kujitokeza kwa wingi kupiga kura Oktoba mwaka huu kwenye uchaguzi mkuu wa Rais,wabunge na madiwani.
Mwenge wa Uhuru umemaliza mbio zake mkoani Ruvuma kwa kupitia miradi katika Halmashauri zote nane ambapo Mei 17 unakabidhiwa katika Mkoa wa Mtwara.
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.