Katika kipindi kisichozidi miezi kumi, Mkoa wa Ruvuma umeandika historia mpya kwenye sekta ya madini baada ya kufanikisha makusanyo ya maduhuli ya Serikali kufikia Shilingi Bilioni 32.5.
Hii ni kwa mwaka wa fedha wa 2024/2025 ulioanza Julai 2024, na makusanyo hayo ni hadi kufikia tarehe 19 Mei 2025, kiasi ambacho ni karibu na lengo la Shilingi Bilioni 33.15 walilopangiwa na Serikali.
Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Ruvuma, Mhandisi Alphonce Bikulamchi, alieleza mafanikio haya mbele ya wanahabari wa Tume ya Madini, akibainisha kuwa matarajio ni Mkoa huo kuvuka lengo hilo kwa zaidi ya asilimia 100 kabla ya kufika mwisho wa mwaka wa fedha mwezi Juni.
Mafanikio haya yanaashiria nidhamu ya ukusanyaji mapato, usimamizi madhubuti, na uwekezaji ulioimarika katika sekta ya madini.
Mhandisi Bikulamchi alitaja biashara ya makaa ya mawe kuwa kichocheo kikuu cha mafanikio hayo, akieleza kuwa makaa ya Ruvuma yamebainika kuwa bora zaidi kitaifa na kimataifa.
Makaa hayo sasa yanauzwa kwa wingi katika nchi za Kenya, Uganda, Rwanda pamoja na masoko ya Bara la Asia na Ulaya, jambo linaloongeza thamani ya madini ya mkoa huo.
Mbali na makaa ya mawe, Ruvuma pia imejaaliwa kuwa na aina nyingi za madini ikiwemo dhahabu, shaba, chuma, urani, madini ya ujenzi na vito.
Wingi na utofauti wa madini haya vimeifanya sekta hii kuwa chanzo kikuu cha mapato kwa Serikali na wananchi wa Mkoa wa Ruvuma, huku fursa mpya za kiuchumi zikiendelea kufunguka kila uchao.
Katika kuhakikisha biashara ya madini inakuwa shirikishi na yenye manufaa kwa pande zote, Serikali kupitia Tume ya Madini imeanzisha masoko rasmi mawili ya madini – Soko la Madini Songea na Soko la Madini Tunduru.
Masoko haya yameongeza uwazi, usalama na usawa kwa wachimbaji na wafanyabiashara wa madini, na kuwezesha Serikali kukusanya mapato kwa njia halali na sahihi.
Mhandisi Bikulamchi aliwataka Watanzania kuchangamkia fursa mbalimbali zilizopo katika mnyororo wa thamani wa sekta ya madini, ikiwemo usambazaji wa teknolojia migodini, huduma za chakula, uchimbaji, uchenjuaji na biashara ya madini.
Ruvuma sasa siyo tu mkoa wa kilimo, bali pia miongoni mwa nguzo kuu za maendeleo ya sekta ya madini nchini.
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.