Katibu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa, Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, amemwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa CCM Taifa, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika shughuli ya kuaga mwili wa Hayati Alhaj Mustafa Mohamed Songambele mkoani Ruvuma.
Akizungumza kwenye hafla hiyo iliyofanyika nyumbani kwa Mzee Songambele Mahenge mjini Songea, Dkt. Nchimbi amesisitiza mchango wa Mzee Songambele katika harakati za kupigania uhuru wa Tanzania, akieleza kuwa alikuwa miongoni mwa waanzilishi wa Chama cha TANU na alishiriki kikamilifu katika kujenga misingi imara ya taifa jipya baada ya uhuru.
"Tuendelee kujifunza kutoka kwa wazee hawa ambao wamefariki wakiona amani na upendo wa Tanzania ukiendelea, heshima pekee tunayoweza kuwapa ni kuendeleza mshikamano, amani na maendeleo ya nchi yetu, tuendelee kujua sisi ni Taifa moja, tuna wajibu wa kupendana na kujiepusha na vishawishi vyote ambavyo vinaweza vikavuruga amani na kuvunja mtangamano wa kitaifa," alisema Dkt. Nchimbi.
Dkt. Nchimbi ameeleza kuwa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia ameguswa sana na msiba huo, akimtaja Mzee Songambele kama kiongozi aliyekuwa na moyo wa kipekee wa kulitumikia taifa kwa hali yoyote hivyo wanaruvuma wana kila sababu ya kujivunia kutokana na mchango wake mkubwa katika kupigania uhuru na kuimarisha maendeleo ya nchi.
Naye Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Kanali Ahmed Abbas Ahmed, ameeleza kuwa kifo cha Mzee Songambele ni pigo kubwa kwa Taifa, akisisitiza kuwa Tanzania imepoteza hazina muhimu ya busara na kumbukumbu hai ya historia yake.
"Hakuwa tu kiongozi bali alikuwa taa na mwelekeo katika giza la ukoloni, aliyesimama kidete kwa ujasiri, hekima, na moyo wa kizalendo katika kuijenga Tanzania mpya alisimama kwa haki, kupitia juhudi zake na viongozi wenzake wa wakati huo, tunauona leo mwanga wa uhuru, umoja, na amani uliodumu kwa zaidi ya nusu karne," alisema Kanali Ahmed.
Kwa upande wake mtoto wa Hayati Alhaj Songambele, Rajab Songambele, amesema kama familia wataendelea kuyaenzi na kuyafanyia kazi mazuri yaliyofanywa na waliyoachiwa na Mzee wao ili yaendelee kuishi.
Hayati Alhaj Mustafa Mohamed Songambele alikuwa ni mmoja wa waanzilishi wa Chama cha TANU ambacho kiliasisi harakati za kudai uhuru akiwa miongoni mwa wanachama wa kwanza 30, na akapewa kadi namba 27, alizaliwa Mei 25, 1925 Bombambili Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma na amefariki akiwa na umri wa miaka 100
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.