Katibu Tawala wa Mkoa wa Ruvuma, Bi. Mary Makondo, ametoa maelekezo muhimu kwa Halmashauri za Mbinga Mji, Mbinga Vijijini na Madaba ili kutekeleza hoja na mapendekezo ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) pamoja na maagizo ya Kamati ya Bunge ya LAAC.
Makondo ametoa maagizo hayo kwa nyakati tofauti wakati akisoma hotuba kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Kanali Ahmed Abbas Ahmed, katika mabaraza ya kujadili hoja za CAG yaliyofanyika katika halmashauri hizo.
Maagizo hayo ni wakuu wa idara na vitengo kushiriki kikamilifu katika kuandaa majibu ya hoja na mpango kazi wa utekelezaji wa hoja za CAG, Menejimenti kuhakikisha taarifa za hesabu za mwisho wa mwaka zinaandaliwa kwa kuzingatia viwango vya kimataifa vya uhasibu vinavyotumika katika sekta ya umma.
Maagizo mengine ni Wakurugenzi wa Halmashauri kuchukua hatua za kinidhamu dhidi ya watumishi watakaobainika kusababisha hoja au hasara kutokana na uzembe, pia Menejimenti kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za fedha na manunuzi, ili kuzuia hoja zisizo za lazima.
Vilevile, ameagiza hoja zote za miaka ya nyuma na maagizo ya LAAC katika halmashauri hizo yashughulikiwe kikamilifu na kufungwa kabla au ifikapo tarehe 30 Septemba 2025.
Kwa mujibu wa ripoti ya CAG kwa mwaka wa fedha ulioishia Juni 30, 2024, Halmashauri ya Mji wa Mbinga ilikuwa na jumla ya hoja 26, kati ya hizo hoja 6 pekee ndizo zilizofungwa na 20 zikiendelea kufanyiwa kazi. Pia, kuna hoja 16 za miaka iliyopita pamoja na maagizo matatu ya LAAC ambayo bado hayajatekelezwa kikamilifu.
Halmashauri ya Wilaya ya Madaba nayo ilipokea hoja 27 ambapo 12 zimefungwa, 15 bado zinaendelea kufanyiwa kazi, huku 10 zikiwa ni za miaka ya nyuma na maagizo mawili ya LAAC bado hayajatekelezwa ipasavyo.
Katika mabaraza hayo, Mkaguzi Mkuu wa Nje wa Mkoa wa Ruvuma, Bw. Nickolas Kilinga, amezipongeza Halmashauri hizo kwa kupata hati safi akisisitiza kuimarisha mifumo ya ukaguzi na udhibiti wa ndani ili kuepuka kuendelea kuwa chanzo cha hoja mpya.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Ruvuma, Komredi Oddo Mwisho, ameeleza kuwa wakaguzi wa ndani ni chujio muhimu katika kugundua mapungufu, hivyo amesisitiza Halmashauri hizo kutoa usaidizi wa kutosha kwa wakaguzi hao ili waweze kufika maeneo mbalimbali, kukagua kwa wakati, na kuchukua hatua zinazostahili ili kupunguza au kuondoa kabisa hoja zinazojitokeza katika taarifa za CAG.
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.