Katika kipindi cha miaka minne tu, Halmashauri ya Wilaya ya Madaba iliyopo mkoani Ruvuma imepiga hatua kubwa ya kimaendeleo kiasi cha kugeuka mfano wa kuigwa kitaifa, hasa katika sekta za elimu na afya.
Mafanikio haya yanatokana na utekelezaji thabiti wa miradi ya kimkakati chini ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Akizungumza na wanahabari mjini Madaba kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Katibu Tawala wa Mkoa, Bi. Mary Makondo, alisema kuwa kuanzia mwaka 2021 hadi 2025, halmashauri hiyo imetekeleza miradi yenye thamani ya shilingi bilioni 20.7, miradi ambayo imeleta mageuzi makubwa ya kijamii na kiuchumi kwa wananchi.
MAPINDUZI MAKUBWA KATIKA ELIMU YA MSINGI NA AWALI
Katika sekta ya elimu ya awali na msingi, ujenzi wa madarasa 68 mapya na ukarabati wa madarasa 25 umetatua changamoto ya msongamano wa wanafunzi darasani.
Aidha, ujenzi wa vyoo 257, nyumba nne za walimu na bweni moja umeongeza ustawi wa mazingira ya kufundishia na kujifunzia.
Pamoja na hayo, madawati 4,426 yamesambazwa katika shule mbalimbali, na hatua ya kujenga Kituo cha Rasilimali kwa Walimu inatajwa kuwa ya kimkakati kwani inalenga kuimarisha uwezo wa walimu kwa njia ya mafunzo endelevu.
"Tulikuwa na changamoto ya madarasa machache, lakini sasa watoto wanakaa kwa nafasi, wanajifunza vizuri, na hata ufaulu umeongezeka. Huu ni ushahidi wa dhamira ya kweli ya Rais wetu kwa elimu.",anasema mwalimu Grace Ngalema wa shule ya msingi Lituta Madaba.
SEKTA YA SEKONDARI YAPAA
Sekta ya sekondari haijabaki nyuma. Madarasa 53 mapya, vyoo 46 na nyumba 13 za walimu zimejengwa. Viti na meza 3,820 vimesambazwa kwa wanafunzi huku shule mbili zikiboresha miundombinu na kuanza kutoa elimu ya kidato cha tano na sita. Maabara 14 zimekamilika na moja kukarabatiwa, hatua inayosaidia kukuza elimu ya sayansi.
Shule mpya nne zimeanzishwa sambamba na ujenzi wa mabweni manne, bweni moja kukarabatiwa, na ukumbi wa chakula kujengwa.
Haya ni mafanikio yanayoongeza upatikanaji wa elimu bora kwa vijana wa Madaba, na kuvutia wanafunzi kutoka maeneo ya jirani.
"Mtoto wangu sasa anasoma sekondari yenye maabara na walimu wanaoishi karibu. Haya mambo yalikuwa kama ndoto miaka michache iliyopita.",anasema Rehema Kapinga Mkazi wa Lilondo
MABORESHO YA KUSISIMUA KATIKA AFYA
Katika sekta ya afya, awamu ya tatu ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Madaba imekamilika, ikijumuisha wodi ya upasuaji na barabara ya ndani yenye urefu wa mita 600.
Huduma za afya zimeimarishwa kwa kujengwa kwa kituo kimoja cha afya na zahanati nne mpya, hatua ambayo imepunguza umbali wa wananchi kutafuta matibabu.
Pia, vifaa vya nishati ya jua vimenunuliwa kwa vituo vya afya ili kuhakikisha upatikanaji wa huduma wakati wote. Serikali imeongeza watumishi wa afya huku magari mawili ya wagonjwa na pikipiki nane zikinunuliwa kwa ajili ya huduma ya afya ya jamii, hasa maeneo ya pembezoni.
"Tumeweza kuongeza huduma za upasuaji, mama wajawazito hawasafirishwi tena kwa umbali mrefu. Tunaweza kuhudumia kesi za dharura hapa hapa Madaba."Anasema mmoja wa madaktari wa hospitali ya Madaba.
MATOKEO CHANYA YANAONEKANA
Mabadiliko haya yameleta matokeo chanya yanayoonekana. Uandikishaji wa wanafunzi umeongezeka, kiwango cha ufaulu kimepanda, na huduma za afya zimeimarika kwa kiasi kikubwa.
Wananchi sasa wanapata huduma kwa wakati na kwa ubora, hali inayowajengea imani kubwa kwa Serikali yao.
Takwimu za Halmashauri zinaonesha kuwa zaidi ya watoto 8,000 wamefaidika na uboreshaji wa miundombinu ya elimu, huku zaidi ya wananchi 70,000 wakipata huduma bora za afya ndani ya kipindi cha miaka minne.
wazi kwamba mafanikio ya Halmashauri ya Madaba si ya kubahatisha, bali ni matokeo ya usimamizi madhubuti wa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.