Kwa macho ya kawaida, barabara ya lami ni njia tu ya kusafiri kutoka sehemu moja hadi nyingine. Lakini kwa anayeipitia barabara ya Mbinga–Mbambabay mkoani Ruvuma , anajikuta akiingia katika sinema halisi ya mandhari ya kuvutia inayochorwa na milima,muonekano wa ziwa Nyasa na anga safi ya bluu.
Barabara hii yenye urefu wa kilometa 66 iliyokamilika kwa kiwango cha lami nzito imegeuka kuwa kivutio cha kipekee cha utalii wa kuona mandhari (scenic tourism), ambapo kila kona inatoa fursa ya kupiga picha za kipekee, hasa pale inapojipinda katikati ya milima ya Livingstone huku ikielekea ziwani Nyasa mjini Mbambabay
Safari kuanzia Mbinga hadi Mbambabay sasa siyo tu njia ya kusafiri, bali ni tukio la kuvutia linalogusa hisia. Mandhari ya kijani kibichi, mashamba ya kahawa na kilimo cha ngolo yanayopamba milima, na upepo mwanana kutoka Ziwa Nyasa, huifanya safari hii kuwa tiba kwa akili na moyo. Wasafiri wengi, hasa watalii wa ndani na nje ya nchi, wameanza kuweka barabara hii kwenye orodha ya maeneo ya kutembelea kutokana na uzuri wake wa asili unaochanganyika na miundombinu bora ya kisasa.
Mbambabay, makao makuu ya ya Wilaya ya Nyasa, hapo awali kilikuwa kijiji tulivu cha uvuvi, sasa inabadilika taratibu kuwa kituo cha utalii wa kimkakati. Hii ni kutokana na barabara hii mpya ambayo imefungua mlango wa uchumi na utalii kwa kuvutia wawekezaji na wageni. Hoteli ndogo ndogo, nyumba za wageni, na waendesha boti za kitalii kwenye Ziwa Nyasa wanaibuka, wakithibitisha kuwa lami si tu barabara bali ni daraja la maendeleo na urithi wa uzuri wa Mkoa wa Ruvuma kuingia katika ramani ya ulimwengu.
Regional Commissioner Office
Anuwani: 1 TUNDURU ROAD, 57180 S.L.P 74,SONGEA, RUVUMA.
Simu: 0252602256
Simu ya Mkononi: KERO PIGA 0800110174
Barua Pepe: ras.ruvuma@tamisemi.go.tz
Copyright ©2017 Ruvuma . All rights reserved.